UFAHAMU UGONJWA WA DENGUE NA NAMNA YA KUJIKINGA.



UFAHAMU UGONJWA WA DENGUE NA NAMNA YA KUJIKINGA.
Homa ya dengue huitwa pia homa inayovunja mifupa
 ( breakbone fever), ni moja ya maradhi ambayo hutokea zaidi msimu wa mvua.
Dengue husababishwa na virusi ambao hukupata baada ya kung’atwa na mbu.



Virusi wanaosababisha ugonjwa wa dengue
Kuna aina 4 za virusi vinavyosababisha Dengue;
DENV-1
DENV-2
DENV-3
DENV-4

Ikitokea umeugua Dengue kutokana na aina moja ya kirusi mwili hutengeneza kinga dhidi ya kirusi hicho lakini kinga hiyo haiwezi kuzuia maambukizi ya aina nyingine ya virusi vya Dengue.
Kwa sababu kuna aina 4 za virusi vya Dengue katika maisha yako unaweza kuugua Dengue hadi mara 4.
Hofu kubwa ni kwamba baada ya kuugua Dengue mara moja maambukizi yanayofuata huja na dalili mbaya zaidi kuliko maambukizi ya mara ya kwanza.

Mbu anayesambaza Dengue ana tabia za kipekee
Mbu anaesambaza dengue huitwa Aedes aegypti;
Mbu huyu ni mdogo mwenye rangi nyeusi na madoa meupe. Kitabia mbu hawa hutaga mayai kwenye maji yaliyotuama hasa kwenye makopo ya maua, hupendelea makopo yenye rangi nzito yaliyo kwenye eneo lenye kiza au matenki yaliyo wazi.
Mbu wa dengue hung’ata vipindi viwili kwa siku, hung’ata asubuhi kabla jua kuchomoza mfano wakati unafungua mlango asubuhi au unatoka kwenda nje ya nyumba, pia hung’ata wakati wa jioni masaa machache kabla ya jua kuzama.
Mda mwingine mbu wa dengue hung’ata usiku maeneo yenye mwanga.
Tofauti ya mbu wa malaria na Mbu wa dengue, ni kwamba mbu wa dengue hung’ata watu bila kushtukiwa kwa sababu huwa hana kelele na hupendelea kuuma sana kwenye magoti na viwiko.


Mbu aina ya Aedes aegypt ambaye husambaza Dengue
Msimu wa mvua na ugonjwa wa Dengue
Dengue ni moja ya magonjwa ambayo huja na mvua ambayo yana jina lisilo rasmi ; Monsoon diseases (Kundi hili la magonjwa hujumuisha na malaria , magonjwa ya kuhara pia).

Wakati wa mvua mbu wanaosambaza ugonjwa wa Dengue huzaliwa kwa wingi pia mbu hawa hukimbilia ndani ya makazi wakati wa mvua hivyo kuwa rahisi kung’ata watu
Ugonjwa wa Dengue huja katika muonekano wa aina mbili
Dengue ya kawaida
Aina hii ya Dengue ndio hupata watu wengi na huwa haina madhara makubwa
Dengue ya kawada huanza siku 4 hadi 10 baada ya kung’atwa na mbu mwenye virusi vya dengue.
Huanza na dalili kama mafua yanayoambatana na homa kali
Homa huambatana na dalili kama:
Kichwa kuuma sana na kuwa na maumivu nyuma ya macho
Maumivu ya misuli na viungo
Mwili kuchoka sana
Kuvimba mitoki (lymph nodes).
Muhimu kufahamu mtoto akipata dengue dalili za mwanzo huwa tofauti na mtu mzima anaweza kuwa na homa tu.
Dengue Kali
Hii ni Dengue ambayo huwa na madhara makubwa huweza kupelekea kifo
Dalili zake huja baada ya dalili za Dengue ya kawaida, hujumuisha
Tumbo kuuma sana
Tumbo kuanza kujaa
Kutapika zaidi ya mara tatu kwa siku
Kutapika damu hata mara moja
Kupoteza fahamu kwa ghafla
Kutoka damu kwa ngozi, puani au masikioni
NB : Katika watu 100 wanaopata dalili mbaya za ugonjwa wa dengue, wagonjwa 90 huwa Watoto wenye umri chini ya miaka 15. Hivyo mtoto anapoumwa dengue inapaswa kuchukulia ugonjwa wake kwa uzito mkubwa na umakini.


Mgonjwa wa dengue hupitia hatua 3 za ugonjwa.
Ugonjwa wa Dengue huwa na hatua 3 za kuumwa ; Hatua ya homa, Hatua ya hatari na hatua ya kupona
01. Hatua ya homa
Hatua hii huanza na homa ya ghafla inayoambatana na maumivu ya kichwa, maumivu ya misuli, maumivu ya maungio kama magoti, na mwili kupoteza maji
02. Hatua ya hatari
Hatua hii huja siku ya 3 hadi 7 baada ya kuanza kuugua.
Hutokana na mishipa ya damu kuanza kufuja plasma na virusi vya Dengue kushambulia seli zinazogandisha damu.

Utaanza kupata damu kwenye ngozi, kutoka damu puani au masikioni, mishipa ya damu kuvuja plasma na kusababisha shock. Hudumu kwa zaidi ya masaa 48.
kuna hatari kubwa ya watu kupoteza maisha katika kipindi hiki endapo kusipopatikana matibabu sahihi.
03. Hatua ya Uponaji
Katika hatua hii mwili huwa na uchovu sana ambao utadumu kwa zaidi ya wiki

Ukali wa ugonjwa wa Dengue hutegemea vitu kadhaa
Umri wako (watoto hupata Dengue kali)
Iwapo una mimba au la (Dengue huwa kali kwa mjamzito)
Iwapo una maradhi mengine kama kisukari, UKIMWI nk
Lishe yako
Iwapo ushawahi ugua dengue kabla (Dengue ya pili huwa kali)
Ubora wa huduma za afya ulizopewa
Uponaji wa Dengue
Ugojwa wa dengue mara nyingi huisha wenyewe, idadi ya vifo huwa ni ndogo katika watu 100 wanaougua dengue ni mtu 1 tu anayeweza kufariki. Tatizo huja iwapo mtu kapata aina ya ugonjwa mkali wa dengue vifo kwa wagonjwa 100 hufikia 5 lakini iwapo hutapata tiba yoyote uwezekano wa kufariki hufikia asilimia 50
USIJITIBU NYUMBANI, NENDA HOSPITALI
Kama una dalili za dengue kama homa kali na kichwa kuuma jitahihidi kuwahi hospitali
Hospitali daktari atachukua maelezo yako na kukupima mwili.
Kipimo cha dengue huchukuliwa kwenye damu , pia kupitia damu daktari atapima wingi wa chembechembe zinazogandisha damu na wingi wa damu.
Ukiwa na dengue utaanzishiwa matibabu ya kuupa sapoti mwili, kupunguza maumivu pia unaweza kuhitaji kuongezewa chembechembe sahani za damu (platelet transfusion)
KANUNI ZITAKAZOSAIDIA MWILI WAKO UWAHI KUPONA
01. Pumzisha mwili kwa kulala
02. Kunywa maji ya kutosha na vimininika vingi kama juisi
03. Tumia dawa za kupunguza homa
04. Usitumie aspirin au ibuprofen




Comments

Popular posts from this blog

Pregnancy Test Timing

CEREBRAL PALSY- IN CHILDREN.